Wafanyaziara walianza matembezi yao ya Arbaeen kutoka eneo la Ra’s al-Bishah, lililo katika maeneo ya mbali kabisa ya kusini mwa Iraq siku ya Ijumaa, kulingana na vyombo vya habari vya Iraq. Safari hii ya kinembo inafanywa chini ya bendera ya "kutoka baharini hadi mtoni" inayorejelea azma yao ya kuvuka masafa makubwa ili kutoa heshima kwa mjukuu wa Mtume Muhammad (SAW), Imam Hussein (AS).
Kwa hakika, washiriki wa kundi hili la wafanyaziara huvuka vyanzo vya maji kwa muda mrefu, wakisisitiza kujitolea kwao bila kuyumbayumba wanapovuka kutoka baharini hadi nchi kavu na kuendelea na Ziara yao kuelekea Karbala.
Wakitembea majini kwa saa nyingi, wafanyaziara hao waliojitolea wanapeperusha kwa fahari bendera zilizopambwa kwa jina la Imam Hussein (AS), wakionyesha waziwazi utiifu wao kwa mafundisho na harakati yake tukkufu.
Arbaeen ni neno la Kiarabu ambalo maana yake ni 40. Katika muktadha huu, ni siku ya 40 tangu maadhimisho ya kuuawa shahidi Imam Hussein (AS) na masahaba wake watiifu tarehe 10 Muharram katika siku ya Ashura. Mtukufu huyo aliuawa shahidi katika mapambano ya Karbala karne 14 zilizopita.
Siku ya Imam Hussein (AS) ya Arbaeen inakuja tarehe 20 Safar, mwezi wa pili wa kalenda ya mwandamo wa Kiislamu.
Baada ya kufa shahidi Imam Hussein (AS) mikononi mwa katili Yazid bin Muawiya, watu ambao walishangazwa na ukatili wa ukoo wa Ummaya walianza kuzuru kaburi lake kutoa heshima zao na tokea wakati huo hadi leo vizazi katika umma wa Kiislamu vimeendeleza utaratibu huo. Kila mwaka idadi ya wafanyaziara katika Siku ya Arabeen inaongezeka ambapo mwaka uliopita idadi hiyo ilivunja rekodi na kufika milioni 21.
3484733