Akizungumza Jumatano, msemaji wa Hamas Abdul Latif al-Qanun amesema utawala haramu wa Israel sasa unazuia ujenzi mpya wa Ghaza baada ya vita vyake vya siku 12 dhidi ya eneo hilo mwezi Mei.
Karibu wapalestina 260, wakiwemo wanawake na watoto waliuawa wakati wa vita hivyo. Ripoti kuhusu uharibifu uliotekelezwa na Israel katika Ukanda wa Ghaza imebaini hasa ya takribani dola milioni 380.
Msemaji wa Hamas amesema hawatasubiri muda mrefu na kwamba utawala wa Kizayuni wa Israel unapaswa kutii matakwa ya Wapalestina na kusitisha mzingiro wa Ghaza.
Tokea mwaka 2007, utawala haramu wa Israel, kwa kushirikiana na Misri, uliweka mzingiro wa anga, nchi kavu na baharini dhidi ya Ukanda wa Ghaza baada ya Wapalestina katika eneo hilo kuichagua kidemokrasia harakati ya Hamas kuongoza eneo hilo. Mzingiro huo umelifanya eneo hilo lenye watu karibu milioni moja na nusu kutajwa kuwa gereza kubwa zaidi la wazi duniani.
Mwezi uliopita, kiongozi mwandamizi wa Hamas Yahya Sinwar alisema wananchi wa Palestina wamekaribia sana kuuvunja mzingiro dhidi ya Ukanda wa Gaza uliowekwa na utawala wa Kizayuni wa Israel kwa kushirikiana na Misri tokea mwaka 2007.
Mbali na mzingiro huo, utawala haramu wa Israel pia umeanzisha vita mara kadhaa dhidi ya Ghaza tokea mwaka 2008 ambapo maelfu ya Wapalestina wakiwemo wanawake na watoto wameuawa.