IQNA

Maombolezo ya Tasua ya Imam Hussein AS yafanyika duniani kwa kuzingatia kanuni za afya

14:27 - August 29, 2020
Habari ID: 3473114
TEHRAN (IQNA) -mamilioni ya Waislamu wa Iran na maeneo mengine ya dunia usiku wa kuamkia leo tarehe 9 Mfunguo Nne Muharram wameshiriki katika vikao, majlisi na shughuli za maombolezo ya Tasua huku wakizingatia kanuni za kiafya ili kuzuia kuenea ugonjwa wa corona.

Sehemu kubwa ya maomboleza hayo ya Tasua ya kukumbuka misiba na masaibu yaliyomfika mjukuu wa Mtume wetu Muhammad SAW, Imam Hussein bin Ali AS, ndugu na mswahaba zake waaminifu huko Karbala nchini Iraq mwaka 61 Hijria, mwaka huu yamefanyika kwa njia ya Intaneti kutokana na janga la ugonjwa wa COVID-19.

Hapa nchini Iran, wananchi Waislamu wa Iran katika miji mbali mbali wamejiunga na kampeni ya "Kila Nyumba ni Husseiniya " huku wakitundika bendera nyeusi katika nyumba zao kuomboleza masaibu ya Imam Hussein na wafuasi wake katika kiwango cha familia. 

Katika siku ya 9 ya mwezi Muharram, wafuasi na wapenzi wa Watu wa Nyumba ya Mtume Mtukufu humkumbuka zaidi Abul Fadhl al Abbas ambaye alionesha ushujaa wa hali ya juu katika mapambano ya Karbala na kuwakumbusha watu ushujaa usio na kifani wa baba yake, Ali bin Abi Twalib AS.

Abul Fadhl al Abbas aliuawa shahidi baada ya kukatwa mikono yote miwili na maadui wa Watu wa Nyumba ya Mtume wetu Muhammad SAW wakiongozwa na Yazid bin Muawiyah.

Watu 72 waliokuweko Karbala wote waliuawa shahidi wakiwa pamoja na kiongozi wao, Imam Hussein bin Ali AS katika mapambano ya haki dhidi ya dhulma na uonevu mapambano ambayo damu ya mashahidi hao ilizishinda panga za maadui.   

3919693

captcha