Duru za habari zimeripoti kuwa utawala wa Kizayuni wa Israel unajiandaa kuupokea ujumbe huo ambao unatazamiwa kufanya uchunguzi kuhusu tuhuma za jinai za kivita ambazo utawala huo haramu unatuhumiwa kuzifanya wakati wa vita vya mwaka 2014 dhidi ya Wapalestina wa Ghaza.
Safari ya ujumbe huo wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ambayo itafanyika hivi karibuni imetokana na ombi la Mwendesha Mashtaka Mkuu wa mahakama hiyo Bi Fatou Bensouda na lengo lake ni kutoa fursa kwa wajumbe wa jopo hilo la ICC kuwa na uelewa wa jinsi mfumo wa vyombo vya mahakama vya utawala wa Kizayuni unavyofanya kazi.
Hapo kabla Mamlaka ya Ndani ya Palestina iliitaka Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ichukue hatua ya kuchunguza jinai za kivita zilizofanywa na utawala wa Kizayuni, hatua ambayo iliwafadhaisha mno viongozi wa utawala huo ghasibu.
Mbali na Mamlaka ya Ndani, shakhsia mbalimbali wa Kipalestina wamekuwa wakitoa wito wa kuchunguzwa jinai za kivita zilizofanywa na jeshi la utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina wa Gaza.
Zaidi ya Wapalestina 2,300 wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto wadogo waliuawa shahidi na maelfu ya wengine walijeruhiwa katika mashambulio ya siku 50 mtawalia yaliyofanywa na jeshi la utawala wa Kizayuni mwaka 2014 dhidi ya Ukanda wa Ghaza.