IQNA

Waislamu India

Ghadhabu nchini India baada ya kuachilia waliofungwa kwa ubakaji na mauaji ya Familia ya Kiislamu

15:05 - August 17, 2022
Habari ID: 3475636
TEHRAN (IQNA) - Wanaume 11 waliohukumiwa kifungo cha maisha jela kwa ubakaji na mauaji ya mwanamke Mwislamu mjamzito na familia yake wakati wa ghasia mbaya katika jimbo la Gujarat nchini India wameachiliwa, na hivyo kuzua hasira dhidi ya serikali ya utaifa wa Kihindu nchini humo.

Bilkis Bano, wakati huo akiwa na umri wa miaka 21 na ujauzito wa miezi mitano, alibakwa huku watu saba wa familia yake wakiuawa wakati wa ghasia za kidini zilizozuka Februari 2002 katika jimbo la Gujarat magharibi.

Mahakama ya Mumbai iliwahukumu watu hao kifungo cha maisha mwaka wa 2008, katika mojawapo ya kesi kuu baada ya ghasia zilizosababisha vifo vya takriban watu 1,000.

Hata hivyo, walipokuwa wametumikia kifungo cha miaka 15 gerezani, mmoja wao - Radheshyam Shah - alikata rufaa kwa Mahakama ya Juu ili kuachiliwa chini ya sera ya serikali ya msamaha.

Wanaume hao waliachiliwa huru katika Siku ya Uhuru wa India siku ya Jumatatu, baada ya serikali ya jimbo inayoendeshwa na chama cha Waziri Mkuu Narendra Modi kuwaachilia, ikitaja "umri wao, asili ya uhalifu, tabia gerezani".

Mahakama kuu mwezi Mei iliitaka serikali ya jimbo hilo kuamua juu ya ombi la Shah na kamati ikaundwa kuchunguza suala hilo, alisema Sujal Mayatra, afisa mwandamizi wa mahakama katika wilaya ya  Panchmahal, ambaye aliongoza kamati hiyo.

"Miezi michache nyuma kamati ilichukua uamuzi wa pamoja wa kuachiliwa kwa wafungwa wote 11 katika kesi hiyo na pendekezo hilo lilitumwa kwa serikali ya jimbo. Tulipokea maagizo ya kuachiliwa kwao jana,” Mayatra alisema.

Ghasia zilizuka katika mji wa Godhra mnamo Februari 2002 baada ya madai kuwa Waislamu waliwaua  wafanyaziara  59 wa Kihindu.

Mauaji hayo ya treni yalifuatia siku za ghasia katika jimbo zima.

Zaidi ya watu 1,000, wengi wao wakiwa Waislamu, waliuawa katika ghasia zilizofuata katika jimbo hilo katika  moja ya matukio mabaya zaidi ya ghasia za kidini katika India ya kisasa.

Bi Bano, kutoka Randhikpur karibu na Ahmedabad, na wengine 15, ikiwa ni pamoja na binti yake mdogo Saleha na mpwa wa siku moja, walikuwa wamekimbia kijiji chao lakini walivamiwa na kundi la Wahindu waliokuwa na mundu, panga na fimbo.

Alibakwa na genge la watu na binti yake wa miaka 3 alinyakuliwa kutoka mikononi mwake na kichwa chake kupasuliwa na mwamba. Wanafamilia sita walifanikiwa kutoroka na wengine saba ambao miili yao haikupatikana baadaye ilitangazwa kuwa wamekufa. Kwa mujibu wa sheria ya India mtu yeyote aliyepotea kwa zaidi ya miaka saba anahesabiwa kuwa amekufa.

Mahakama maalum mnamo Januari 2008 iliwahukumu wahalifu hao 11 hao kifungo cha maisha kwa makosa ya ubakaji na mauaji.

3480128

Kishikizo: india waislamu modi
captcha