IQNA

Jinai za Israel

Makanisa ya Methodist Marekani yapinga sera za Israel za ubaguzi wa rangi

15:55 - June 18, 2022
Habari ID: 3475392
TEHRAN (IQNA)- Jumamosi, Juni 11, 2022 huko Manchester, NH, jimboni New Hampshire Marekani, Kongamano la New England la Makanisa ya Methodist ilipitisha kwa wingi azimio lenye kichwa “Kutambua na Kupinga Ubaguzi wa Rangi Katika Ardhi Takatifu.”

Katika upigaji kura, asilimia 88% walipiga kura ya "ndiyo" na 12% "hapana" ambapo watu 354 walipiga kura kwa njia ya intaneti huku wengine wakishiriki katika upigaji kura ndani ya ukumbi. Mkutano huo ulijumuisha majimbo yote ya eneo la New England kaskazini-mashariki mwa Marekani isipokuwa nusu ya magharibi ya Connecticut.

Azimio hilo liliazimia “kwamba Mkutano wa Mwaka wa New England…unatambua kwamba serikali ya Israeli imeanzisha mfumo wa ubaguzi wa rangi (apathaidi), unathibitisha kwamba ubaguzi wa rangi ni kinyume na ujumbe wa Injili, ambao unapinga udhalimu huu na uonevu kwa namna yoyote ile inayojidhihirisha.”

Taarifa hiyo iliendelea pia kusema "kwamba mkutano huo unaitaka serikali ya Marekani kuweka masharti ya ufadhili wa Marekani kwa Israel kuwa ni Israel kuvunja mfumo wake wa ubaguzi wa rangi na kutekeleza haki zote zinazostahili Wapalestina chini ya sheria za kimataifa."

Katika kumalizia washiriki wa kongamano hilo waliwataka “makasisi na waumini wote wa Kanisa la Methodist: a) kusikiliza sauti za Wapalestina kuhusu hali yao…na b) kuungana na kuunga mkono watu wote wenye mapenzi mema wanaotafuta haki kwa ajili ya watu wote katika Ardhi Takatifu (Palestina inayokaliwa kwa mabavu na Israel)".

Azimio hilo lilitanguliwa na matamshi kadhaa kuhusu hali halisi ya maisha ya Wapalestina katika Ardhi Takatifu na kubainisha kuwa, mashirika kadhaa ya kutetea haki za binadamu yametoa ripoti zinazobainisha mfumo wa utawala wa kibaguzi wa Israel, ikiwemo B. 'Tselem mwaka 2021, Human Rights Watch mwaka 2021, na Amnesty International mwaka 2022.

Azimio hilo lilibainisha kuwa mwaka wa 1988 “Kanisa la Muungano wa Methodisti limetangaza kwa nguvu kupinga uhalifu wa ubaguzi wa rangi au apathaidi, na kuuita 'uzushi' na 'dhambi' ambayo inapaswa kulaaniwa bila shaka - ndani ya Kusini mwa Afrika na nchi jirani na duniani kote. ' ”

Madhehebu mengine ya Kikristo yanaelekea upande huo huo wa kupinga ubaguzi wa rangi wa utawala bandia ya Israel.

4064884

captcha