IQNA

Zaidi ya Waislamu Milioni Mbili waanza Ibada ya Hija

21:35 - August 19, 2018
Habari ID: 3471636
TEHRAN (IQNA)- Zaidi ya Waisalmu milioni mbili kutoka maeneo yote ya dunia wamejumuika katika mji mtakatifu wa Makka kuanza Ibada ya Hija mwaka huu.

Ibada ya Hija imeanza Jumapili ambapo Mahujaji wameanza harakati kutoka Makka kuelekea Minaa huku baadhi wakitembea kwa miguu na wengine kwa mabasi na magari. Masafa baina ya Makka na Mina ni takribani kilometa nane.

Huku hayo yakijiri, imebainika kuwa Saudi Arabia inakidhi nakisi ya bajeti yake ya mwaka kwa kuzidisha gharama za ibada ya Hija, suala ambalo limewakasirisha mahujaji kutoka nchi mbalimbali hususan mahujaji kutoka Misri.

Omar Marwan mwakilishi wa serikali ya Misri katika masuala ya Bunge na kiongozi wa msafara wa Hija wa Misri amesema kuwa, idadi ya mahujaji wa nchi hiyo walioelekea Makka kwa ajili ya kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu imepungua kwa asilimia 20 ikilinganishwa na mwaka uliopita wa 2018. Ameongeza kuwa idadi ya mahujaji wa Misri mwaka huu imepungua kutoka elfu 80 hadi elfu 65. 

Wakati huo huo Ahmed Ibrahim ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Hija ya Misri amesema kuwa, idadi ya Wamisri waliokwenda kufanya umra mwaka huu wa 2018 imepungua kutoka mahujaji laki 3 na 80 hadi elfu 50 na kwamba sababu yake ni matatizo ya kiuchumi na kupanda kwa gharama za Hija. Ibrahim amesema uamuzi wa Suaudi Arabia wa kupandisha gharama za ibada ya Hija umewafanya Wamisri wengi washindwe kwenda kutekeleza ibada hiyo muhimu. 

Kupungua kwa bei ya mafuta na gharama za vita vya Saudi Arabia dhidi ya Yemen vinatajwa kuwa sababu kuu za kupandishwa gharama za ibada ya Hija zinazowazuia Waislamu kutoka nchi mbalimbali kwenye kutekeleza faradhi hiyo huko Makka. 

3739697

captcha