IQNA

Mohammad Salah wa Liverpool kufunga Saumu ya Ramadhani masaa 18 katika siku ya Fainali ya Ulaya

13:16 - May 22, 2018
Habari ID: 3471526
TEHRAN (IQNA)- Pamoja na kuwa atashiriki katika mechi muhimu zaidi ya soka katika maisha yake, yamkini nyota wa Liverpool Mohammad Salah akafunga saumu ya Ramadhani katika siku ya mechi na Real Madrid ya Fainali ya Mabingwa wa Ulaya.

Salah ambaye ni Mmisri , amenukuliwa na tovuti ya El-Ahly.com  akisema hatavunja saumu yake ya Ramadhani katika siku ya fainali hiyo itakayochezwa Jumamosi Mei 26 katika mji muu wa Ukraine, Kiev Uwanja wa NSC Olimpiyskiy.

Katika msimu huu, hivi sasa masaa ya kufunga Saumu ya Ramadhni mjini Kiev ni takribani 18.

Bado haijabainika iwapo kocha wa Liverpool Jurgen Kloop ana mpango maalumu wa lishe kwa ajili ya Salah lakini kocha wa Timu ya Soka ya Misri Hector Cuper amesema ameshachukua hatua kuhakikisha kuwa Salah na wachezaji wengine watapata lishe sahihi wakati wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kabla ya Fainali za Kombe la Dunia ambazo zitaanza Juni 14 nchini Russia.

Timu ya Liverpool haijatangaza wazi kuwa iwapo Salah na mchezaji mwingine Mwislamu katika timu hiyo, Sadio Mane, wanafunga Saumu ya Ramahdani kabla ya Fainali za Mabingwa wa Ulaya.

Hivi karibuni Mufti Mkuu wa Misri Sheikh Shawki Allam alisema wachezaji wa Timu ya Taifa ya Soka ya Misri wana idhini ya kuahirisha saumu ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani katika siku za kabla ya Kombe la Dunia nchini Russia kutokana na joto kali katika wakati huu wa kujitayarisha kwa ajili ya mechi hizo. Aliongeza kuwa Waislamu wanaosafiri wanaruhusiwa kutofunga Saumu ya Ramadhani na kulipa siku hizo baadaya hatahivyo aliongeza kuwa kuwa wachezaji ambao watahisi wanaweza kufunga saumu basi wafanya hivyo.

Nchini Uingereza Mohammad Salah amepata umashuhuri kutokana na umahiri wake katika soka na maadili yake mema. Sala si Mwislamu jina tu, bali ni kijana ambaye hutekeleza mafundisho ya Kiislamu ikiwemo kuswali sala tano kwa siku. Yeye huonekana akiswali akiwa ameandamana na wachezaji wenzake Waislamu ambao ni Sadio Mané na Emre Can na kila anapopachika bao wavuni husujudu kama njia ya kumshukuru Allah SWT kwa kumpa kipaji alichonacho.

3465905

captcha